Friday, March 18, 2016

KUHUSU KIFO CHA SHABIKI HUYU WA SOKA

BAADA ya jana jioni kutokea kifo cha shabiki wa Azam, Emmanuel Machibe, kwenye Uwanja wa Azam Complex Chamazi, uongozi wa timu hiyo umetokeza na kusema wanajisikia unyonge na kifo cha shabiki huyo.

Machibe, aliyekwenda uwanjani hapo kwa ajili ya kushuhudia mchezo wa timu yake dhidi ya Stand United, alikutana na kifo hicho baada ya kukanyagwa na gari.

Taarifa iliyowekwa kwenye mtandao wa klabu hiyo ilisema, Azam, inapenda kutuma salamu za rambirambi kwa familia ya Machibe, kufuatia kifo cha mpendwa wao.

Taarifa hiyo ilisema Azam, imesikitishwa na kifo cha kijana huyo na inapenda kutoa pole kwa familia, ndugu, jamaa na marafiki pamoja na wapenzi wote soka nchini katika kipindi hiki kigumu cha maombolezo.

“Licha ya timu yetu kupata ushindi, lakini hatukufurahishwa na
tukio la kuondokewa na mpendwa wetu Machibe ambaye ni mkazi wa Kiwalani jijini Dar es Salaam.

“Tunatoa pole kwa Watanzania wote ambao ni wana michezo baada ya kuondokewa na shabiki wetu Machibe, ambaye ni kati ya mashabiki bora na tunaungana na familia ya marehemu (Machibe) kwenye kipindi hiki kigumu walichonacho” ilisema taarifa hiyo.

Machibe, anatokea katika kikundi cha ushangiliaji cha Azam kutoka Tawi la Mpira Kazi lililopo Magomeni jijini Dar es Salaam.

No comments:

Post a Comment

Comment here