Tuesday, June 7, 2016

WANAFUNZI CHUO CHA ST JOSEPH WATAKIWA KUSOMA HADI DIPLOMA

WANAFUNZI wa Chuo Kikuu cha St Joseph (SJUIT) Kampasi ya Arusha (kilichofutiwa usajili), waliokuwa chini ya programu ya shahada ya miaka mitano ya ualimu wa sayansi, wametakiwa kusoma ngazi ya cheti au stashahada. Kama watataka kusoma ngazi ya juu, watapaswa kuomba upya udahili.Aidha, Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi imesema wanafunzi waliokuwa wakipata mkopo kutoka Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB), mikopo yao pia imesimamishwa.

 

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Simon Msanjila alitoa agizo hilo jana kupitia taaarifa kwa vyombo vya habari. Profesa Msanjila alisema hatua hiyo, inatokana na kubainika kwamba wanafunzi hao hawastahili kusoma shahada na pia hawakustahili kupewa mkopo.

“Tunawafahamisha wanafunzi wa SJUIT waliokuwa kwenye programu ya miaka mitano kwamba watatakiwa kuishia daraja la cheti na stashahada… Kama wanafunzi hao watataka kuendelea na masomo ya juu, watatakiwa kuomba upya,” ilisema taarifa hiyo.

Februari 25, mwaka huu, Wizara kupitia Tume ya Vyuo Vikuu (TCU) baada ya kujiridhisha kuwa Kampasi ya Arusha ya Chuo Kikuu cha Mt. Joseph Tanzania imepoteza sifa na vigezo vya kuendelea kutoa elimu ya chuo kikuu, ilifuta kibali cha kuanzishwa kwake.

No comments:

Post a Comment

Comment here